Header Ads Widget

WATEMI WA KISUKUMA,VIONGOZI WA TAS WAIBUKIA KITUO CHA WATOTO WENYE UALBINO BUHANGIJA - SHINYANGA



Watemi wa Kisukuma Kanda ya Ziwa Victoria na viongozi wa Chama Cha Watu Wenye Ualbino nchini Tanzania( Tanzania Albinism Society -TAS) wamefanya usafi wa mazingira kisha kula chakula cha pamoja na watoto wenye ualbino wanaolelewa katika kituo cha Buhangija katika manispaa ya Shinyanga.

Watemi hao wakiongozwa na Katibu Watemi wa Kisukuma Kanda ya Ziwa, Mtemi Charles Balele Itale wa Bujashi wilaya ya Magu mkoa wa Mwanza walitembelea kituo hicho leo Jumamosi Julai 8,2017. 


Mwenyekiti wa Chama Cha Watu Wenye Ualbino nchini Tanzania -TAS taifa, Nemes Temba alisema chama hicho kimekuwa na ushirikiano mkubwa na machifu wa kanda ya ziwa hicho kuamua kushiriki nao katika kufanya usafi wa mazingira katika kituo cha Buhangija. 

“Malengo ya kuja hapa kwanza ni kuunga mkono serikali ya awamu ya tano kuhusu masuala ya usafi,pili ni kuwapa ujumbe watoto hawa kuwa wawe na utamaduni wa kufanya usafi hata wanaporudi kwenye familia zao,tatu tumekuja kula chakula cha pamoja na watoto hawa ili kuonesha kuwa tuko pamoja nao”,alieleza Temba. 

Temba alitumia fursa hiyo kuiomba serikali kuchunguza utitiri wa mashirika yaliyoanzishwa nchini ambapo sasa yapo zaidi ya 10 na kufuatilia vituo mbalimbali vilivyoanzishwa kwa lengo la kuwahudumia watu wenye ualbino hususani watoto kwani sasa vipo takribani 20 lakini wahusika wa vituo hivyo hawasaidii walengwa. 

Temba alisema mashirika mengi yamekuwa yakijikita katika kupiga vita mauaji ya watu wenye ualbino huku yakisahau kuwa watu wenye ualbino wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa elimu na saratani ya ngozi ambayo imekuwa ikiua watu wengi wenye ualbino. 



 Katibu Watemi wa Kisukuma Kanda ya Ziwa, Mtemi Charles Balele Itale wa Bujashi wilaya ya Magu mkoa wa Mwanza alimpongeza mwenyekiti wa Chama cha Watu wenye Ualbino kuwakutanisha pamoja katika kituo hicho. 
“Juhudi hizi zinaonesha jinsi tunavyowatambua,tunavyowapenda na tunavyowajali watu wenye ualbino,kwa hiyo katika nafasi zetu za nyadhifa mbalimbali tunajitahidi kuelimisha na kuwezesha jamii iwatambue,iwajali,iwapende na kuwapokea katika jamii na watoto warudi kwenye familia zao na kuishi kama watoto wengine”,alieleza Mtemi Balele. 
“Nimefurahishwa na taarifa ya uongozi wa kituo hiki kuwa sasa watoto wameanza kwenda likizo kuwaona wazazi wao,hili ni jambo jema sana,Sisi machifu tuna jukumu letu ni kuielimisha jamii iwapokee,iwakubali,isiwanyanyase,isiwanyanyapae hivyo sisi kwa kushirikiana na TAS tutashirikiana katika kutafikia hayo malengo”,aliongeza Mtemi Balele. 
Awali akizungumza katika kituo hicho,Mwalimu Mlezi wa Shule ya Msingi Buhangija, Frola Kakutebe alisema kati ya watoto wenye ualbino 140,waliopo katika kituo hicho,72 wameenda likizo na 68 wamebakia kituoni baada ya shule kufungwa kinyume na miaka ya nyuma ambapo watoto hao walikuwa hawaendi likizo kuonana na ndugu zao. 
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo,Selemani Kipanya aliiambia Malunde1 blog kuwa,sasa Kituo hicho kimepoteza sifa ya kuitwa kituo bali ni shule kwani tofauti na siku za nyuma hivi sasa watoto wanaoishi hapo wote wanasoma shule na wanaishi katika mabweni yaliyopo katika shule hiyo.
ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI

Download/Pakua App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

إرسال تعليق

0 تعليقات